Friday 1 February 2013

WABUNGE WA UPINZANI WATOKA NJE YA BUNGE

Pichani: Mhe. Mbatia (kushoto) na Mhe. Tundu Lissu (Kulia) wakiongea katika mkutano wao na waandishi wa habari, mara baada ya kususa kikao cha bunge. Mhe. Lissu ni Mnadhimu wa kambi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Singida kupitia CHADEMA.


Siku ya Ijumaa tarehe 1.2.2013, wabunge wa kambi ya upinzani waliamua kususia  kikao cha Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa kutoka nje, ikiwa ni alama ya kuonesha kutoridhishwa na jinsi kiti cha Spika kisivyowatendea haki wabunge wasiokuwa wa chama tawala, na kinavyokandamiza hoja za kulisaidia taifa hasa pale zinapotolewa na wabunge wa kambi ya upinzani.
Hatua hiyo ilikuja baada ya Mheshimwa James Mbatia (NCCR-Mageuzi) kudai aoneshwe nakala ya mtaala wa elimu uliopo, ili aitimishe hoja yake kuhusu udhaifu uliomo katika elimu mfumo wa elimu ya Tanzania. Badala ya kusikiliza ombi hilo, Naibu Spika wa Bunge, Mheshimiwa Job Ndungai alimkatalia Mbatia na kumlazimisha ahitimishe hoja yake binafsi aliyoitoa siku moja kabla. Mbatia alikataa kufanya hivyo, ndipo ndipo yeye pamoja na wabunge wa vyama vya NCCR, CHADEMA, na TLP wakaamua kutoka nje.  Baadaye wabunge hao walifanya mkutano na waandishi wa habari mjini Dodoma, na kueleza hatua watakazozichukua, kuwa ni pamoja na kumtaka waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dr. Shukuru Kawambwa ajiuzulu au awajibishwe na mamlaka iliyomteua, kwani alikuwa amelindanganya Bunge kwa kusema mtaala ulioandikwa upo. Walisema endapo hata mamlaka iliyoko juu ya waziri Kawambwa haitamuwajibisha, basi watapiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu.

No comments:

Post a Comment